Pesatu ni jukwaa la habari, elimu ya kifedha, na ujasiriamali Tanzania. Pata taarifa mpya za biashara, uwekezaji, ajira, kilimo, mitindo, na burudani kwa Kiswahili, pamoja na mwongozo wa kufanikisha mafanikio yako.
Nchi zilizoendelea zimetakiwa kutimiza ahadi yao ya kutoa dola za marekani bilioni 500, sawa na dola bilioni 100 kila mwaka kwa ajili ya kuzisaidia nchi zinazoendelea kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabianchi katika kipindi cha miaka mitano, kuanzia mwaka 2020 hadi mwaka 2025.
Waziri wa Fedha Dkt. Mwigulu Nchemba amesema hayo wakati akichangia hoja katika Mkutano wa Ngazi ya Juu wa Mawaziri uliojadili namna ya kupata fedha kwa ajili ya kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi, pembezoni mwa Mkutano wa 29 wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Umoja wa Mataifa kuhusu Mabadiliko ya Tabianchi (COP-29) unaofanyika katika Mji wa Baku, nchini Azerbaijan
Alisema kuwa ripoti ya Mkutano wa COP28, uliofanyika Dubai mwaka jana, inaonesha kwamba kuna kasi ndogo katika kutimiza ahadi ya Mkataba wa Paris katika kuhamasisha upatikanaji ama uchangiaji wa dola 100 bilioni ambapo kuna pengo la takribani dola bilioni 60 kila mwaka hali inayo ziathiri nchi zinazoendelea katika kupanga mipango ya maendeleo.
Aidha, Dkt. Nchemba alisema kuwa Tanzania inataka kuwe na uwazi namna fedha hizo dola bilioni 100 zinazotakiwa kutolewa kila mwaka kwa nchi zinzoendelea ili kuweka uwajibikaji kulingana na Mkataba wa Paris kuhusu suala hilo la kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.
Alisema kuwa mabadiliko ya Tabianchi ni janga linalobomoa Uchumi wa nchi zinazoendelea na kushauri matamanio na ahadi zinazotolewa na mataifa makubwa yawekwe katika vitendo ili kuzinusuru nchi zinazoendelea kutokana na madhara yanayosababishwa na mabadiliko hayo ya tabianchi.
Dkt. Nchemba alisema kuwa Tanzania ni miongoni mwa nchi zinazoendelea iliyoathirika na matokeo hasi ya mabadiliko ya tabianchi na inajitahidi kutumia rasilimali zake kukabiliana na athari hizo ikiwemo kurejesha miundombinu iliyoharibiwa na mafuriko lakini fedha hizo za ndani hazitoshelezi mahitaji.