Tsh Bilioni 14.3 kutumika ujenzi wa maabara ya kuchunguza madini
Takribani Shilingi bilioni 14.3 zinatarajiwa kutumika katika ujenzi wa maabara kubwa na ya kisasa ya uchunguzi wa sampuli za madini ambayo itakuwa ni kubwa kuliko zote kwa nchi za Afrika Mashariki na Kati na ambayo itatoa huduma ya kimaabara kwa ubora na kwa uharaka kwa wadau wa sekta ya madini nchini.
Hayo yamesemwa na Waziri wa Madini Anthony Mavunde wakati wa kuweka jiwe la msingi la ujenzi wa maabara ya kisasa ya uchunguzi wa sampuli za madini katika eneo la Kizota,Jijini Dodoma.
“Tunamshukuru Rais Dkt. Samia S. Hassan kwa kuwa kinara wa mageuzi makubwa ya sekta ya madini na kwa kuandika historia ya ujenzi wa maabara hii ya kisasa miaka 100 baadaye tangu kuanzishwa kwa Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa madini(GST) mwaka 1925,” amesema Mavunde.
Amesema leo Tanzania inaandika historia ya kuanza kwa ujenzi wa maabara kubwa ambayo itafungwa mitambo na vifaa vya kisasa katika kutoa huduma za kimaabara ndani na nje ya nchi.
“Huu ni ukombozi mkubwa kwa wadau wa sekta ya madini katika kupata taarifa sahihi za kimaabara kwa wakati na zenye ubora wa hali ya juu na kuongeza, nii imani yangu maabara hii itachochea ukuaji na maendeleo ya sekta ya madini,” amesema Mavunde.
Soma: Sekta ya madini yafikia mchango wa 10.1% Pato la Taifa
Naye, Kaimu Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini(GST) Dkt. Notka Batenze amesema Maabara hiyo ya kisasa ya uchunguzi wa sampuli za madini italeta tija kwa wadau wa Sekta ya Madini na kurahisisha upatikanaji wa huduma hii muhimu kwa maendeleo ya sekta ya madini.
Gharama za ujenzi wa maabara hiyo unatarajiwa kuwa Shilingi Bilioni 14.3 na muda wa ujenzi wa kukamilika maabara ni siku 690.
Machi 2025, Afisa Madini Mkazi wa Mbogwe, Mhandisi Jeremiah Hango alisema zaidi ya leseni 4,000 zipo katika utaratibu wa kutolewa katika maeneo manne ya Mkoa wa Kimadini Mbogwe mkoani Geita, huku wazawa na wawekezaji kutoka nje wakitakiwa kuchangamkia fursa zilizopo mkoani humo.
Mhandisi Hango alisema maeneo yaliyotengwa ni Nyamikonze ambapo leseni 81 ziliweza kugawiwa kwa wachimbaji wadogo, kuna eneo la Mwamakiliga leseni 27 zilitengwa.
“Maeneo mengine ni Bukombe kijijini leseni 140 na sasa hivi mchakato wa Kigosi ambapo takribani leseni 4,000 kutengwa,” amesema Mhandisi Hango.
Amesema zoezi la ugawaji bado linaendelea na kwamba fursa zilizopo zikitumiwa vizuri serikali itaweza kukusanya kiasi kikubwa cha maduhuli.
“Nawakumbusha wamiliki wa leseni ambao wameshikilia leseni katika mkoa wetu wa kimadini Mbogwe wazifanyie kazi leseni hizo, nyingi hawazifanyii kazi, kuna leseni za utafiti ambapo ukienda saiti watu wanaofanya utafiti ni wachache sana.
Vile vile niwakumbushe kama leseni hizo hawatazifanyia kazi tutazifuta na kuwapa watu wengine wenye nia ya kufanyia kazi leseni na sio kuzishikilia,” amesema.
Soma: Tanzania kununua helikopta kuchunguza madini ardhini